Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Uchukuzi

BILIONI 34 ZATUMIKA KUKARABATI MV LIEMBA

Imewekwa: 17 Aug, 2026
BILIONI 34 ZATUMIKA KUKARABATI MV LIEMBA

Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, leo tarehe 15 Agosti, 2026 ameshuhudia zoezi la majaribio ya meli ya MV Liemba katika Ziwa Tanganyika mkoani Kigoma baada ya kukamilika kwa ukarabati wake mkubwa uliogharimu Shilingi  bil 34

Akizungumza na wanahabari Prof. Mbarawa amesema ukarabati huo ulianza baada ya Serikali kumpata mkandarasi mwaka 2023 na  kueleza kuwa kurejea kwa MV Liemba kutasaidia wananchi wa Kigoma, Katavi, Rukwa na maeneo mengine kupata huduma muhimu ya usafiri wa majini

Prof. Mbarawa amesema meli hiyo imefanyiwa maboresho makubwa, ambapo injini mbili, jenereta tatu, chumba cha uendeshaji pamoja na maeneo ya abiria vimefanyiwa maboresho na kuwekwa katika hali mpya

Aidha, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwezesha ukarabati huo, akisema lengo ni kuhakikisha MV Liemba inaendelea kutoa huduma kwa wananchi kwa miaka 50 na zaidi

Waziri Mbarawa amesema Serikali itaendelea kusimamia majaribio na ukaguzi wa kina, na baada ya kukamilika kwa taratibu zote, MV Liemba inatarajiwa kuanza kutoa huduma kwa wananchi kuanzia Septemba 1, 2026.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa TASHICO Bw. Eric Hamissi amesema majaribio hayo ni muhimu katika kuhakikisha mifumo yote ya meli inafanya kazi kwa ufanisi na usalama kabla ya kuanza rasmi kutoa huduma kwa wananchi.

Naye Mha. Elias Kivara anayesimamia ukarabati na majaribio ya MV Liemba amesema majaribio hayo yanahusisha injini, jenereta, mfumo wa uendeshaji, kuongeza na kupunguza kasi pamoja na uwezo wa meli kusimama kwa wakati unaotakiwa.